Page 166 - Fasihi_Kisw_F5
P. 166

Fasihi ya Kiswahili  kwa Shule za Sekondari




               Shughuli 6.9
              Tumia vyanzo vya mtandaoni, maktabani  au vinginevyo, kueleza  kanuni
              zinazoongoza utunzi wa shairi.

          FOR ONLINE READING ONLY
              Kanuni za kutunga mashairi
              Mashairi  huwa na sifa za kipekee  ambazo  huyafanya kutofautiana  na tanzu
              nyingine za fasihi. Kwa mantiki hiyo, kuna mambo muhimu ambayo hayana budi
              kuzingatiwa wakati wa utunzi wa mashairi. Mambo hayo ni lugha ya kishairi,
              muundo, muwala, taswira na ishara, mtindo na utoshelevu.

              (a)  Lugha ya kishairi
              Mashairi hutumia lugha ya mkato na kibunifu kama vile matumizi ya uwekevu,
              tamathali za semi, misemo na nahau. Mwandishi anatakiwa kuzingatia vipengele
              hivi ili kuleta mvuto wa shairi lake. Katika uandishi wa shairi, mtunzi ana uhuru
              wa kukiuka kanuni za kisarufi ili kukidhi mahitaji ya ushairi.

              (b)  Muundo
              Muundo wa mashairi unatofautiana na muundo wa matini nyingine za kifasihi
              kwa sababu ya vipengele mbalimbali kama vile beti, mistari, mizani na miundo
              mingine kulingana na aina ya shairi. Mwandishi hana budi kuandika shairi lenye
              muundo  unaosadifu  mahitaji  ya  shairi  lake;  na  kwa  njia  hii  anaweza  kuibua
              muundo mpya tofauti na ile iliyozoeleka. Katika ushairi wa Kiswahili, miundo
              iliyozoeleka ni ile ya kimapokeo na ya kisasa.

              (c)  Muwala
              Mtunzi hana budi kuzingatia kipengele  cha muwala ambacho hushughulikia
              uwiano mzuri  wa sehemu  zote  za shairi.  Muwala huweza kupatikana  kupitia
              uzingatiaji wa mtiririko wa fikra katika umbo mahsusi la shairi ambao husaidia
              kujenga mantiki ili kuwasilisha maudhui yaliyokusudiwa. Ushikamani wa kifikra
              hutokea baina ya mshororo na mshororo, ubeti na ubeti, na hatimaye, shairi zima.

              (d)  Taswira na ishara
              Mtunzi wa shairi haelezi mambo moja kwa moja bali huyafumbata anayotaka
              kuyaeleza ndani ya taswira na picha zinazotumia ishara. Matumizi haya huathiri
              hisia za wasomaji kama vile za upendo, huzuni, furaha, na hasira. Mbinu hii ya
              matumizi mazuri ya lugha ya picha na ishara humfikirisha msomaji wa shairi kwa
              kumfanya azifasili taswira na ishara hizo ili kupata maana iliyokusudiwa.

              (e)  Mtindo
              Mshairi huwa na uwanja mpana wa kutumia  mitindo mbalimbali  kiuandishi.
              Anaweza kutumia mtindo wa kimapokeo unaofuata kanuni za urari wa vina na
              mizani au wa kisasa unaokiuka kaida na kanuni hizo.


                     Kitabu cha Mwanafunzi                                           155
                        Kidato cha Tano



                                                                                            23/06/2024   17:54
     FASIHI YA KISWAHILI KITABU CHA MWANAFUNZI KIDATO CHA TANO.indd   155                   23/06/2024   17:54
     FASIHI YA KISWAHILI KITABU CHA MWANAFUNZI KIDATO CHA TANO.indd   155
   161   162   163   164   165   166   167   168   169   170   171