Page 23 - Fasihi_Kisw_F5
P. 23

Fasihi ya Kiswahili  kwa Shule za Sekondari




              (c)  Visasili
              Visasili ni hadithi zinazoelezea chimbuko au asili ya jamii, ukoo, au kundi fulani.
              Huelezea pia tamaduni mbalimbali na namna jamii fulani ilivyofika katika eneo
              fulani. Kadhalika, visasili huelezea  na kufafanua masuala ya kimaumbile  na
          FOR ONLINE READING ONLY
              kiimani  yanayomhusu  na kumsumbua  binadamu  kama  vile  maradhi  na kifo.
              Visasili hueleza pia maana ya maisha na hatima ya mwanadamu kulingana na
              imani za jamii inayohusika. Kwa kawaida, visasili huheshimiwa na kuaminiwa
              na wanadamu, na huhusishwa na kuwa vielelezo vya miviga na ibada zao. Mfano
              wa kisasili ni hadithi za mataifa mbalimbali kuhusu kuumbwa kwa ulimwengu
              na  vilivyomo.  Mfano  mzuri  ni  hadithi  ya Wakikuyu  ya  “Gikuyu  na  Mumbi”
              ambayo inapatikana katika kitabu cha  Naushangilia Mlima Kenya (Kenyatta,
              1966), simulizi ya “Asili ya jina la Wakinga” kutoka kwa Wakinga, na simulizi ya
              “Adamu na Hawa” kutoka Mashariki ya Kati ambayo inapatikana katika Biblia
              na Kurani.

              Mfano wa Kisasili


               Asili ya Jina la Wakinga
               Wenyeji  wa jamii  ya Wakinga  wanapatikana  Nyanda  za  Juu Kusini katika
               eneo lenye vilima, uoto mzuri wa asili na vijito vinavyotiririka kama mkufu
               usio na mwisho. Wenyeji wa jamii hii walikuwa na shughuli mbalimbali tangu
               enzi za zamani. Walijishughulisha na ufuaji chuma, viazi, ngano na njegere.
               Palipo na ustawi hapakosekani adui. Jamii hii ilikuwa na mbinu zake za siri
               za ulinzi ambazo kila mwanajamii alifundishwa katika makuzi yake. Wakinga
               walikuwa na maadui na walipigana vita mara kwa mara na kuvishinda vita
               hivyo. Adui alipovamia  ardhi ya  Wakinga,  kiongozi  alijitokeza  na kupiga
               kelele  ‘Vakinga  Vakinga!’ (maana yake jihadhari)  akiwa amepanda  juu ya
               kilima. Baada ya hapo kila mwanajamii alitambua kuwa hiyo ni vita na kila
               mmoja  aliwajibika  kupambana. Wazee  waliongoza  jamii  nzima  kwa kutoa
               ushauri na kuombea ushindi, vijana walichukua silaha za kivita,  wanawake
               na watoto walikimbilia kwenye mahandaki. Huo ndio mwanzo wa Wakinga
               kuitwa Wakinga kulikotokana na sauti hiyo ya tahadhari.


              (d)  Vigano
              Vigano  ni  hadithi  fupifupi za  kifasihi  simulizi.  Mafunzo  yake  hutolewa  kwa
              kutumia lugha ya picha kama ilivyo kwa methali. Hadithi hizi zina hadhi ya
              methali ingawa hutumia taswira pana kuliko methali. Kimsingi, hadithi za namna
              hii hutolewa kama vielelezo, hasa wakati wa mazungumzo au maongezi. Lengo
              kuu huwa ni kumkanya na kumfunza anayesikiliza.



                12                                                 Kitabu cha Mwanafunzi
                                                                     Kidato cha Tano



                                                                                            23/06/2024   17:54
     FASIHI YA KISWAHILI KITABU CHA MWANAFUNZI KIDATO CHA TANO.indd   12
     FASIHI YA KISWAHILI KITABU CHA MWANAFUNZI KIDATO CHA TANO.indd   12                    23/06/2024   17:54
   18   19   20   21   22   23   24   25   26   27   28