Page 53 - Fasihi_Kisw_F5
P. 53

Fasihi ya Kiswahili  kwa Shule za Sekondari




              (a)  Tanzia
              Tanzia ni tamthiliya zenye tukio au matukio ya kuhuzunisha; nayo huhusika na
              mambo yenye uzito kifikra na kihisia, katika maisha ya binadamu. Mhusika mkuu
              ambaye kwa kawaida ni mtu maarufu mwenye kupewa sifa nyingi zinazovutia,
          FOR ONLINE READING ONLY
              hukabiliwa  na  shida au tatizo. Tatizo  hilo  ni  kama  lile  linaloweza  kumkabili
              mtu yeyote. Ijapokuwa mhusika huyo hujitahidi  kulitatua  tatizo hilo, hali ya
              ulimwenguni na tabia ya kibinadamu humfanya asiweze kufaulu, na mwishowe
              hushindwa. Kwa hiyo, mwisho wa tamthiliya hizi ni masikitiko, maanguko na
              hasara kwa mhusika mkuu au jamii. Mfano wa tanzia ni tamthiliya ya Kinjeketile
              (Hussein, 1969) na Kifo Kisimani (wa Mberia, 2001).

              (b)  Ramsa
              Ramsa, ambayo hujulikana pia kama komedia au futuhi, hukusudia kufurahisha
              au kuchekesha, na huwa na mwisho mwema. Sifa ya kufurahisha na kuchekesha
              haimaanishi kwamba tamthiliya za aina hii hazina maudhui mazito. Tamthiliya
              hizi hushughulikia masuala mbalimbali ya msingi kama vile uzembe, uzalishaji
              mali, siasa, mapenzi na ndoa. Utani, mzaha na kejeli hutumika katika kuchekesha.
              Kupitia uchekeshaji huo, jamii, watawala na watu binafsi hukosolewa. Mhusika
              mkuu wa ramsa si lazima awe mtu maarufu. Anaweza kuwa mtu wa kawaida
              au anaweza  kuwa mtu  wa nasaba  duni, lakini  hubeba  matendo  ya ucheshi
              yanayobeba maana nzito. Mhusika huyu akifanikiwa, wasomaji au watazamaji
              hufurahi. Mfano mzuri wa ramsa ni tamthiliya ya Mfalme Juha (Topan, 1971) na
              Aliyeonja Pepo (Topan, 1973).

              (c)  Tanzia ramsa
              Hii ni tamthiliya yenye mseto wa maudhui ya kuhuzunisha na kufurahisha. Mifano
              ya tamthiliya hizi ni Kaptula la Marx (Kezilahabi, 1999), Pambo (Muhando,
              1975), Masaibu ya Ndugu Jero (Soyinka, [mf.] Yahaya, 1974), Mabepari wa
              Venisi  (Shakespeare [mf.] Nyerere, 1969),  Wakati Ukuta  (Hussein, 1967) na
              Amezidi (Mohamed, 1995).


              (d)  Melodrama
              Melodrama ni tamthiliya yenye matumizi mengi ya muziki na uimbaji wa nyimbo.
              Inafanana sana na tanzia ingawa, mara nyingi, nguli wa melodrama huibuka na
              ushindi. Dhamira za melodrama huzungumzia mvutano kati ya wema na uovu
              au ubaya. Matukio yake husisimua sana na mwendo wa msuko wake huwa wa
              harakaharaka. Wahusika wake huvutia lakini hawana sifa za kishujaa. Aghalabu,
              mwishoni, mhusika mwema huweza kupata ushindi.





                42                                                 Kitabu cha Mwanafunzi
                                                                     Kidato cha Tano



                                                                                            23/06/2024   17:54
     FASIHI YA KISWAHILI KITABU CHA MWANAFUNZI KIDATO CHA TANO.indd   42                    23/06/2024   17:54
     FASIHI YA KISWAHILI KITABU CHA MWANAFUNZI KIDATO CHA TANO.indd   42
   48   49   50   51   52   53   54   55   56   57   58