Page 60 - Fasihi_Kisw_F5
P. 60

Fasihi ya Kiswahili  kwa Shule za Sekondari




              (a)  Riwaya za kijamii
              Hizi ni riwaya zinazosawiri maisha na matatizo ya kawaida ya kijamii. Matatizo
              hayo huweza kuwa ya kifamilia, kimahusiano, kitabaka, kisiasa na kiutamaduni.
              Maudhui mengine ni mgongano kati ya ukale na usasa, kati ya maisha ya mjini na
          FOR ONLINE READING ONLY
              ya vijijini na migogoro ya kifamilia. Wahusika wake, aghalabu, huwa halisi ambao
              wanapatikana  katika  jamii.  Hivyo, huifanya  riwaya iwe inaishi  wakati  wote,
              yaani haichuji. Aina hii ndiyo yenye idadi kubwa ya riwaya. Mifano ya riwaya za
              aina hii ni Siku ya Watenzi Wote (Robert, 1968), Rosa Mistika (Kezilahabi, 1971),
              Titi la Mkwe (Banzi, 1972) na Nyota ya Rehema (Mohamed, 1978).

              (b)  Riwaya za kisaikolojia
              Hizi ni riwaya zinazosaili nafsi ya mhusika. Hudodosa fikra, hisia, mawazo, imani,
              hofu, mashaka, matumaini na matamanio ya mhusika binafsi. Vilevile, hudadisi
              athari za mambo hayo kwa mhusika na labda jamii yake. Hueleza mikinzano
              ya ndani ya mhusika kinafsi, kiakili na kijinsia. Baadhi ya riwaya za aina hii ni:
              Rosa Mistika (Kezilahabi, 1971), Kiu (Mohamed, 1972), Ukiwa (Mkangi, 1973),
              Kichwamaji (Kezilahabi, 1974), Tata za Asumini (Mohamed, 1990), na Mhanga
              Nafsi Yangu (Mohamed, 2012).

              (c)  Riwaya za sira
              Hizi ni riwaya ambazo husimulia habari za maisha ya mtu. Riwaya za aina hii
              zimegawanyika katika makundi mawili: riwaya za kitawasifu na za kiwasifu.

              (d)  Riwaya za kitawasifu
              Riwaya  za  kitawasifu  ni  zile  zinazotumia  nafsi  ya  kwanza,  yaani  mwandishi
              anaelezea  mwenyewe kuhusu  maisha yake tangu kuzaliwa kwake hadi muda
              wa kuandika riwaya husika; au hueleza kipande cha maisha yake ambacho sio
              lazima  kiwe  hadi  anapoandika.  Mwandishi  hueleza  matukio  ambayo  huona
              yanasisimua  na huenda hayatokei  kwa wengine. Kwa kuyaeleza,  anadhani
              yanaweza kuwasaidia wasomaji. Riwaya ya aina hii huweka kumbukumbu au
              historia ya maisha ya mtu binafsi. Mifano ya riwaya za aina hizi ni Maisha Yangu
              na Baada ya Miaka Hamsini (Robert, 1949 na 2003), Mbali na Nyumbani (Shafi,
              2013) na Nasikia Sauti ya Mama (Walibora, 2015).


              (e)  Riwaya za kiwasifu
              Riwaya za kiwasifu ni zile zinazotumia nafsi ya tatu, yaani mwandishi husimulia
              maisha ya mtu mwingine. Mfano wa riwaya za wasifu ni Wasifu wa Siti Binti
              Saad (Robert, 1967).






                     Kitabu cha Mwanafunzi                                            49
                        Kidato cha Tano



                                                                                            23/06/2024   17:54
     FASIHI YA KISWAHILI KITABU CHA MWANAFUNZI KIDATO CHA TANO.indd   49                    23/06/2024   17:54
     FASIHI YA KISWAHILI KITABU CHA MWANAFUNZI KIDATO CHA TANO.indd   49
   55   56   57   58   59   60   61   62   63   64   65