Page 24 - Historia_Maadili
P. 24

Hata hivyo, wakati Waingereza walipopewa idhini ya kutawala Tanganyika na
          Zanzibar, wananchi walikuwa tayari wanajishughulisha na kilimo cha mazao ya
          biashara, kama vile buni iliyolimwa Moshi na Bukoba. Pamba nayo ilikuwa ikilimwa
          katika maeneo ya Mwanza, Shinyanga, Morogoro na Pwani. Shughuli za biashara
          wakati wa utawala wa Waingereza zilifanywa na watu wa jamii ya Kiasia, hasa
          Waarabu na Wahindi. Jamii hii ilijihusisha na biashara ya kununua mazao kutoka
        FOR ONLINE READING ONLY
          kwa wakulima na kuyauza kwa makampuni ya kibepari ya Wazungu. Pia, walifanya
          biashara ya kuuza bidhaa mbalimbali zilizoagizwa kutoka Ulaya magharibi na
          Marekani. Watanganyika na Wazanzibari hawakuruhusiwa kushiriki katika biashara
          wakati wa utawala huo. Waingereza, Wagiriki na Wahindi ndio waliofanya biashara
          ya kuagiza na kusafirisha nje ya koloni bidhaa mbalimbali. Waarabu na Wahindi
          walifanya biashara ya maduka ya rejareja maeneo ya mijini na vijijini.

          Kwa upande wa viwanda, Waingereza hawakuwekeza sana katika viwanda vikubwa
          ila walianzisha viwanda vidogo vidogo. Serikali ya Waingereza ilikusanya malighafi
          kama vile mazao ya kilimo, madini na mifugo na kuzisafirisha kwenda kwenye
          viwanda vyao huko Uingereza. Bidhaa zilizozalishwa huko zililetwa na kuuzwa
          kama bidhaa za viwandani hapa nchini. Viwanda vilivyokuwa hapa vilijikita zaidi
          katika kuchakata malighafi ili kupunguza uzito kabla ya kusafirishwa. Kwa mfano,
          viwanda vya kusindika buni, katani, karanga na pamba, pamoja na viwanda vya
          kukaushia tumbaku vilianzishwa. Waingereza pia waliendeleza uchimbaji wa
          madini kwa kupanua migodi iliyoachwa na Wajerumani na kuanzisha mingine
          mipya, kama migodi ya chumvi huko Uvinza na Ulanga na migodi ya dhahabu
          huko Chunya na Geita.

          Usafirishaji na uchukuzi ni baadhi ya shughuli za kiuchumi zilizopewa kipaumbele
          na serikali ya Waingereza. Juhudi za kufufua miundombinu iliyoharibiwa na vita
          zilifanyika, ikiwemo kukamilisha ujenzi wa reli katika baadhi ya maeneo kama vile
          reli kutoka Tabora hadi Mwanza na reli kutoka Moshi hadi Arusha. Pia, bandari na
          usafiri wa meli katika Ziwa Tanganyika na  ziwa Viktoria uliimarishwa. Lengo la
          kuimarisha usafirishaji na uchukuzi lilikuwa kurahisisha usafirishaji wa malighafi
          kutoka maeneo ya uzalishaji hadi bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara  tayari
          kwa kusafirishwa Ulaya. Vilevile, njia hizi za usafirishaji ziliwezesha bidhaa za
          viwandani kusafirishwa kutoka bandarini kuelekea masoko ya maeneo ya bara.

          Kwa upande wa Zanzibar, Waingereza waliwatumia Waarabu na Wahindi kuendeleza
          masilahi yao ya kiuchumi. Waarabu walipewa ardhi yenye rutuba kwa ajili ya kilimo
          cha mikarafuu na minazi, wakati Wazanzibari wengi walipewa ardhi isiyo na rutuba.
          Wahindi walipewa jukumu la kusimamia biashara, hivyo walijenga shule ili kuendeleza
          uzoefu wao. Mnamo mwaka 1923, shule kwa ajili ya watoto wa Kihindi zilianzishwa.


                                                  16




                                                                                        03/10/2024   18:15:08
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   16                                         03/10/2024   18:15:08
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   16
   19   20   21   22   23   24   25   26   27   28   29