Page 32 - Historia_Maadili
P. 32

Jamii za Kitanzania ziliundwa na makabila mbalimbali, kila moja likiwa na mila,
          desturi, maadili na miundo ya kijamii ya kipekee. Hivyo, jamii hizi zilijikuta zikikinzana
          na mifumo ya maadili ya kikoloni, ambayo ilikuwa na madhumuni ya kudhoofisha
          mila na imani za wenyeji, kama vile imani za jadi, sherehe za kimila kama ndoa na
          tohara na elimu ya jadi kama jando na unyago. Pia, taratibu na mienendo ya kimila
          kama kuishi kijamaa, uwajibikaji, heshima na uongozi wa kijadi vilidhoofishwa.
        FOR ONLINE READING ONLY
          Ukoloni ulipoingia na kujiimarisha, uliingiza mifumo mipya ya kimaadili na kijamii,
          ambayo mara nyingi ilikinzana na mila za wenyeji. Mifumo hiyo ya kikoloni ililenga
          kuzidhoofisha mila na imani za kiasili, zikiwemo dini za jadi na mila na desturi zao.
          Mtazamo wa kikoloni ulipuuzia vipengele vya kuishi kidugu katika jamii za wenyeji
          na badala yake ulisisitiza ubinafsi na maadili mengine ya kikoloni ambayo yalikuwa
          mapya kwa jamii za Kitanzania.



           Kazi ya kufanya 2.1


            Umealikwa kuwakilisha shule yako katika semina kuhusu mada isemayo Vijana
            na Maadili. Andaa muhtasari utakaoutumia kuwasilisha mawazo yako kwa
            kutumia dondoo zifuatazo:

             (a)  Umuhimu wa maadili katika jamii; na

             (b)  Nafasi ya vijana katika kuyaenzi na kuyaendeleza maadili katika jamii.



          Maadili ya jamii za Kitanzania wakati ukoloni unaingia

          Katika jamii za Kitanzania, misingi ya maadili ilijengwa juu ya umoja, ushirikiano
          na mshikamano miongoni mwa wanajamii. Vilevile, utunzaji wa mazingira, heshima
          kwa wazee na viongozi na utunzaji na ulezi wa familia na jamaa vilikuwa ni sehemu
          muhimu ya maadili hayo. Aidha, nidhamu, uaminifu na utii kwa mila, miiko na
          desturi za jamii zilikuwa nguzo kuu za maadili. Hata wakati wa ukoloni, misingi hii
          iliendelea kudumishwa kwa kiasi kikubwa na jamii za Kitanzania licha ya changamoto
          zilizokuwepo.

          Ukoloni ulipoingia katika jamii za Kitanzania mwishoni mwa karne ya 19, mfumo
          wa maadili uliokuwepo, ambao ulilenga kujenga mshikamano wa kijamii, kuheshimu
          tamaduni na kuishi kwa amani na utulivu. Mfumo huu ulijikita katika mila na desturi
          zilizorithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine, ukizingatia ushirikiano, utu, haki
          na heshima. Ingawa kulikuwa na makabila mbalimbali Tanzania, mila na desturi za
          makabila hayo zilifanana kwa kiasi kikubwa.



                                                  24




                                                                                        03/10/2024   18:15:09
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   24
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   24                                         03/10/2024   18:15:09
   27   28   29   30   31   32   33   34   35   36   37