Page 39 - Historia_Maadili
P. 39

utoaji elimu katika kila jamii, ambapo elimu hiyo ilitolewa wakati wote na kwa
          vitendo. Mafunzo ya jando na unyago yaliandaliwa kwa madhumuni ya kuwaandaa
          vijana kwa maisha ya utu uzima na kuchukua majukumu ya kijamii. Mafunzo haya
          yalitolewa kwa njia mbalimbali kama vile kilimo, ufugaji, uwindaji, mapishi, ujenzi
          na uvuvi. Vilevile, elimu ilitolewa kupitia hadithi, methali na uzoefu wa vitendo.
        FOR ONLINE READING ONLY
          Hii iliwawezesha wanajamii, hususani watoto na vijana, kupata maarifa stahiki na
          ujuzi muhimu.

          Mamlaka za kikoloni zilianzisha mifumo rasmi ya elimu iliyofuata mfumo wa elimu
          na maadili ya kimagharibi ya Ulaya. Shule za wamisionari zilifundisha masomo
          yanayohusu maadili ya kwao, huku mara nyingi zikikataa na kupinga mila, tamaduni
          na desturi za Kitanzania kuendelea kutumika miongoni mwa wanajamii. Kwa mfano,
          wanafunzi mara nyingi waliadhibiwa kwa kuzungumza lugha zao za asili shuleni na
          walisisitizwa kujifunza na kufuata desturi na maadili ya kimagharibi yaliyohifadhiwa

          na wazungu kupitia mfumo wa ukoloni.

          Hali kadhalika, mfumo wa elimu ya kikoloni ulisababisha mabadiliko makubwa
          ya kiutamaduni. Watanzania wengi waliosoma shule hizi walifuata njia za kufikiri,
          kuvaa na kuenenda Kizungu, ambazo zilipingana na mila, desturi na maadili ya
          Kitanzania. Watumishi wa serikali ya kikoloni walilazimika kuvaa mavazi maalumu
          kama sare kwa mfano maaskari na manesi. Watumishi wengine walivaa mavazi
          yaliyoelekezwa na idara zilizohusika kama ya elimu, mahakama na wahudumu wa
          ofisi. Hali hii ilijenga matabaka kati ya wasomi walioelimika, ambao walikuwa

          wameshikamana zaidi na maadili ya kikoloni na wale ambao hawakupata elimu ya
          kikoloni na waliodumisha njia za maisha za jadi. Kuwagawa Watanzania lilikuwa
          moja ya malengo makuu ya wakoloni katika sera yao ya “wagawe ili uwatawale”.
          Hivyo, hali hii ilichangia mmomonyoko wa kimaadili na kiutamaduni na hivyo
          kusababisha kuenea na kukua kwa kanuni za kiutamaduni za kimagharibi na hivyo
          kudunisha maadili ya Kitanzania.

          Afya: Kabla ya ujio wa wakoloni, jamii za Kitanzania zilikuwa na mifumo mbalimbali

          ya utoaji huduma za afya, kulingana na tamaduni na mila za jamii iliyohusika. Ingawa
          hakukuwa na hospitali au vituo vya afya kama vilivyo sasa, hii haimaanishi kuwa
          huduma za afya hazikuwepo. Kulikuwa na matumizi ya dawa za asili zilizotokana
          na mimea na vifaa vingine kama vile mafuta au maji, ambazo zilitumika kutibu
          magonjwa mbalimbali. Dawa hizi zilipatikana kwa urahisi katika mazingira yao.
          Kulikuwa na wataalamu waliobobea katika masuala ya afya kama vile waganga
          wa mitishamba, wakunga na ngariba waliokuwa na jukumu la kutibu na kuzuia


                                                  31




                                                                                        03/10/2024   18:15:10
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   31                                         03/10/2024   18:15:10
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   31
   34   35   36   37   38   39   40   41   42   43   44