Page 61 - Historia_Maadili
P. 61

Matumizi ya silaha duni dhidi ya silaha bora za Wajerumani
          Katika sehemu kubwa ya Tanzania, wananchi walioshiriki katika mapambano
          hawakufanikiwa kuuangusha utawala wa kikoloni kwa sababu Wajerumani walitumia
          silaha bora zaidi kuliko zile zilizotumiwa na wananchi. Kwa mfano, Wajerumani
          walitumia mizinga na bunduki, wakati wananchi walitumia pinde, mishale, ngao,
          mawe, marungu na majambia.
        FOR ONLINE READING ONLY

          Usaliti
          Baadhi ya viongozi wa jadi waligeuka kuwa vibaraka wa serikali ya kikoloni. Katika
          maeneo mengi, baadhi ya jamii za Kitanzania ziliungana na Wajerumani kupigana
          na jamii zingine za Kitanzania. Hii ilisababisha jamii nyingi kushindwa vita, kwani
          jamii jirani zilizoungana na Wajerumani ziliwasaidia kufichua udhaifu na nguvu za
          jamii hizo na hivyo kurahisisha ushindi kwa Wajerumani. Kwa mfano, Wasangu na
          Wabena waliungana na Wajerumani kutoa siri na kupigana na Wahehe. Vivyo hivyo,
          katika jamii za Wachaga, Mangi Mandara/Rindi aliungana na Wajerumani kumshinda
          Mangi Sina.


          Maandalizi duni
          Wananchi hawakuwa na maandalizi mazuri ya vita ikilinganishwa na wavamizi wa
          kikoloni. Wavamizi walikuwa na muda mzuri wa kujiandaa kwa vita, wakati jamii
          nyingi za Kitanzania zilijikuta katika vita ghafla, mara baada ya kuona wavamizi
          tayari wamevamia. Jamii za Kitanzania zilikuwa hazijamjua vyema adui yao, hali
          iliyochangia kushindwa kwao. Maandalizi mazuri ya Wajerumani yaliwafanya
          washinde vita kwa urahisi.


          Teknolojia duni ya mawasiliano
          Wajerumani walikuwa na teknolojia nzuri ya mawasiliano na usafiri, ambayo ilirahisisha
          mawasiliano kati ya maeneo mbalimbali. Kwa mfano, waliweza kutumia telegramu
          kutuma taarifa za vita kuhusu vifaa na wanajeshi kwa haraka. Hii ilikuwa ngumu kwa
          jamii za Kitanzania, ambazo zilitegemea njia za jadi za mawasiliano zilizochukua
          muda mrefu kufikisha ujumbe kwa walengwa. Pia, Wajerumani walitumia magari na
          vyombo vingine vya usafiri vilivyowarahisishia harakati zao, huku wapiganaji wa
          Kitanzania wakitumia muda mrefu kutembea kwa miguu.


          Uchumi dhaifu

          Jamii nyingi za Kitanzania zilikuwa na uchumi dhaifu ambao usingeweza kuhimili
          vita kwa muda mrefu. Uchumi wao ulitegemea kilimo na biashara ndogo ndogo
          zilizofanywa na wanajamii, ambao wakati wa vita walihitajika kuenda vitani badala
          ya kuendeleza shughuli zao za kiuchumi. Hii ilimaanisha kuwa kipato chao kidogo
          kingeweza kusaidia mapigano kwa muda mfupi tu. Wakati huo huo, Wajerumani
          walikuwa na uchumi imara uliowawezesha kuhimili vita kwa muda mrefu, kwani
          nchi ya Ujerumani ilikuwa na uwezo wa kuwasaidia kifedha.


                                                  53




                                                                                        03/10/2024   18:15:14
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   53                                         03/10/2024   18:15:14
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   53
   56   57   58   59   60   61   62   63   64   65   66