Page 65 - Historia_Maadili
P. 65

chini ya Sultani Jamshid bin Abdullah Al Said tarehe 10 Desemba, 1963. Waziri Mkuu
          wa Serikali ya Sultani aliitwa Mohamed Shamte kutoka ZPPP. Hata hivyo, harakati
          za ukombozi wa Waafrika walio wengi zilifanikiwa kupitia Mapinduzi Matukufu
          ya tarehe 12 Januari, 1964. Hivyo, ilikuwa ni jukumu muhimu kwa wananchi wa
          Tanganyika na Zanzibar kuanzisha harakati za kuudai uhuru na kujikomboa kutoka
          katika ukoloni wa Kisultani na Kiingereza.
        FOR ONLINE READING ONLY

          Misingi ya kudai uhuru wa Tanganyika na Zanzibar

          Harakati za kudai uhuru wa Tanganyika na Zanzibar zilianza mara tu baada ya
          kuanzishwa kwa serikali za kikoloni. Watanzania wengi hawakupendezwa na tawala
          za kikoloni na hivyo wakaanzisha mapambano na harakati za kupinga tawala hizo.
          Zipo sababu kadhaa zilizowafanya Watanzania kuanzisha harakati za kudai uhuru
          wao.  Hii ni pamoja na kuupinga unyonyaji wa mali na rasilimali za wananchi, sera
          za kibaguzi na za kinyonyaji za wakoloni, ukandamizaji wa Waafrika, kuzilinda mila
          na desturi dhidi ya tamaduni za kigeni na kutaka kuishi kwa amani katika taifa huru
          linaloongozwa na viongozi wa Kitanzania. Sababu hizi zinafafanuliwa zaidi katika
          sehemu zifuatazo:

          Unyonyaji wa mali na rasilimali: Mfumo wa kikoloni ulikuwa wa kinyanyasaji
          na kinyonyaji. Watanzania walinyonywa katika nchi yao. Mathalani, walifanya kazi
          maeneo mbalimbali kama vile mashambani, migodini na sehemu nyingine za nchi bila
          kupata ujira unaostahili.  Pia, mfumo wa kikoloni uliwalazimisha wananchi kulima
          mazao yaliyoletwa na wakoloni kwa ajili ya viwanda vyao vilivyopo Ulaya. Sera za
          kikoloni zilizokuwa za kinyonyaji zilisababisha Watanzania kuachana na malengo ya
          kufanya kazi kwa ajili ya kuzalisha mazao yaliyoletwa na wakoloni. Hali hii ilijenga
          msingi mmojawapo katika harakati za kudai uhuru wa Tanganyika na Zanzibar.

          Sera za kibaguzi: Katika kipindi cha ukoloni, sera mbalimbali za kibaguzi zilianzishwa
          kupitia huduma za jamii na ajira. Kwa mfano, wananchi walibaguliwa katika kupata
          huduma za kijamii kama vile; afya, elimu na makazi. Wazungu, Waarabu na Waasia
          walipewa huduma bora wakati Waafrika wakipewa huduma duni au kutokupewa
          kabisa. Vilevile, kulikuwa na ubaguzi katika kupata ajira zenye hadhi. Kwa ujumla,
          Waafrika walipewa kazi za usaidizi na zile za ngazi ya chini sana zilizosababisha
          kulipwa  ujira mdogo usioendana na uzito wa kazi walizokuwa wakifanya. Hali hii
          ilisababisha baadhi ya wananchi kususia bidhaa za kikoloni kama njia ya kupinga
          sera za kibaguzi za wakoloni.

          Ukandamizwaji wa Waafrika: Wakoloni walipofika walianza kupora ardhi nzuri
          ya uzalishaji mali kutoka kwa wenyeji. Hivyo, ili watu waweze kuishi, iliwalazimu
          kufanya kazi katika mashamba ya wakoloni kwa ujira mdogo na wakati mwingine bila
          malipo. Pia, serikali za kikoloni ziliwatoza kodi wananchi kwa nguvu na kuwafanyisha
          kazi katika mashamba yao kwa ujira mdogo. Vilevile, katika maeneo mengine,


                                                  57




                                                                                        03/10/2024   18:15:14
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   57                                         03/10/2024   18:15:14
   HISTORIA YA TANZANIA NA MAADILI F2.indd   57
   60   61   62   63   64   65   66   67   68   69   70